WAFANYAKAZI WA CHUO KIKUU MZUMBE MBEYA WAAZIMIA KUMKOMBOA MTOTO WA KIKE

Zikiwa ni siku kadhaa tangu kuhitimishwa kwa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Dunia, Wafanyakazi wa Chuo Kikuu Mzumbe Ndaki ya Mbeya, wameanzisha kampeni mahususi ya ujenzi wa Bweni la Wanafunzi wa kike, kwa lengo la kutanua wigo wa nafasi za malazi ya wanafunzi wa kike chuoni hapo.

Akizindua harambee ya ujenzi wa Bweni la watoto wa kike katika halfa ya chakula cha jioni iliyoandaliwa na Menejimenti ya Ndaki ya Mbeya, Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Prof. William Mwegoha, ambaye pia alikuwa mgeni rasmi, alisema ameguswa sana kwa namna wafanyakazi katika Kampasi hiyo walivyoguswa na kuamua kuwa wa kwanza kuchangia harambee hiyo, ambayo imepangwa kuhusisha wadau wote wakiwemo watanzania wenye mapenzi mema na watakaoguswa na harambee hiyo. 

“ Najua kuwekuwa na mipango ikiendelea kwa ushirikiano na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mhe. Homera, ya kuwa na harambee kama hii kwa kuanza na mkoa wa Mbeya ya kuchangia ujenzi wa bweni la wanafunzi wa kike na baadae kampeni hii itakwenda kwenye hatua zingine. Lakini kwa dhati kabisa, nimeguswa zaidi kwa moyo wenu wa upendo na uzalendo mkubwa mliouonyesha kwa watoto wetu, rafiki zetu, wadogo zetu  na kuamua kuonyesha njia, kwa kuzingatia ule msemo “ charity begins at home”.  Alisema

Amesema, atahakikisha Kampasi zingine (Morogoro na Dar es Salaam)  nao wanashiriki katika kampeni hiyo, ili kuwa mfano katika mwendelezo wa kampeni za aina hiyo zilizopangwa na menejimenti ya Chuo katika kuhakikisha wadau wote muhimu wanashirikishwa katika kufikia malengo ya ujenzi wa Bweni la Watoto wa Kike ambao wengi wao wamekuwa wakiishi nje ya Kampasi kutokana na nafasi za malazi kutotosheleza idadi halisi ya wanafunzi wanaojiunga na chuo hicho.

Harambee hiyo iliyofanyika katika hoteli ya GR, Mbeya mjini, ilihudhuriwa na wafanyakazi wa chuo hicho waliotoa ahadi ya zaidi ya Tshs. Mil 39 na fedha taslimu Tshs. 230,500/=.

Akimkaribisha mgeni rasmi, Rasi wa Ndaki ya Mbeya, Prof. Henry Mollel, amesema, tayari michoro ya jengo imekamilika, pamoja na kufanya makisio ya thamani halisi ya jengo ambalo litagharimu kiasi cha Tshs. Bil 5. Amesema jengo hilo litakuwa na Ghorofa saba, na hadi kukamilika litakuwa na uwezo wa kulaza wanafunzi 800 kwa mara moja.

“Binafsi nimefarijika sana kuona ndoto hii inaanza kutimia; kama sote tunavyofahamu changamoto za watoto wa kike ni nyingi. Si kwamba tumewaacha kabisa wavulana hapana, lakini kutokana na maisha tunayopitia kila siku tumegundua watoto wa kike ambao baadhi yao hujiunga na chuo chetu wakiwa katika umri mdogo, ni vema wakafirikiwa kwanza kupata malazi ya uhakiki na salama, wakati tunabuni miradi mingine ya ujenzi wa mabweni kwa ajili ya wavulana pia” alisisitiza Prof. Mollel

Kwa sasa Ndaki ya Mbeya ina jumla ya wanafunzi 3411 wanaosoma fani mbalimbali kuanzia ngazi ya Stashahada, Astahahada, Shahaza za Awali na Shahada za Umahiri, kati ya hao wanafunzi 400 tu ndiyo waliopata nafasi ya malazi chuoni ikiwa ni sana na asiliamia 11.7% ya idadi ya wanafunzi waliosoma chuoni hapo. Ndaki ya Mbeya ilianzishwa mwaka 2006 takribani miaka 17 iliyopita ikiwa na wanafunzi 395 tu. Idadi ya wanafunzi imeendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka kutokana na idadi ya programu zinazoanzishwa na kufundishwa, pamoja na kupanda kwa ubora wa Elimu inayotolewa.

 

 

Address

MBEYA CAMPUS COLLEGE
Forest Area - Mbeya City
Mzumbe University
P.O.Box  6559, Mbeya, Tanzania
Tel: +255 (0) 252502863 /57/58
Fax: +255 (0) 252502862
email: This email address is being protected from spambots. You need JavaScript enabled to view it.